Tangaza Nasi

Burundi yatangaza Mei 17 kuwa tarehe ya kura ya maoni



Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi ametangaza Mei 17 kuwa tarehe ya kufanyika kura ya maoni ya kuifanyia mabadiliko katiba ya nchi.
Kwa mujibu wa dikrii iliyosainiwa jana Jumapili, kampeni za kuunga mkono au kupinga marekebisho hayo ya katiba zitaanza wiki mbili kabla ya tarehe ya zoezi lenyewe.
Dikrii hiyo imesema shakhsia na vyama vya siasa vinavyotaka kushiriki kwenye kampeni za kura hiyo ya maoni sharti visajiliwe na Tume Taifa ya Uchaguzi CENI, kati ya Machi 23 na Aprili 6.
Iwapo asilimia 50 ya wapiga kura wataunga mkono mabadiliko hayo ya katiba, watakuwa wamemsafishia njia Rais Nkurunziza mwenye umri wa miaka 54 na ambaye amekuwa madarakani tokea mwaka 2005, kusalia uongozini hadi mwaka 2034.
Februari mwaka huu, Gaston Sindimwo, Makamu wa Kwanza wa Rais wa nchi hiyo, sambamba na kuzindua zoezi la kuwaandikisha watu milioni 5 katika daftari la kudumu la wapiga kura, alitangaza kuwa kura hiyo ya maoni ingefanyika mwaka 2020, pamoja na uchaguzi mkuu.

Hakuna maoni

Inaendeshwa na Blogger.